Kuhusu Sisi
KKKT DAYOSISI YA KASKAZINI KATI
"Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema BWANA, ni mawazo ya amani wala si mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho"

Yeremia 29:11
"Onjeni mwone ya kuwa BWANA yu mwema; Heri mtu yule anayemtumaini"

Zaburi 34:8
"Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake."

Warumi 8:28
Historia ya dayosisi ya kaskazini kati
Dayosisi ya Kaskazini kati ya KKKT ilianza mwaka 1973, wakati huo ikijulikana kwa jina la Sinodi Mkoani Arusha, iliyoongozwa na Mchungaji Mesiaki Kilevo; akiwa kiongozi wa kwanza wa Sinodi ikiwa na Washarika 30,000, Sharika 20 na Mitaa 110.
Kiongozi wa Pili wa Sinodi alikuwa hayati Askofu Dkt Thomas Olmorijoi Laiser kuanzia mwaka 1980 hadi mwaka 1986. Mwaka huo wa 1986 Sinodi ilibadilika kuwa Dayosisi Mkoani Arusha na Askofu wa kwanza akawa hayati Askofu Dkt Thomas Olmorijoi Laiser.
Mwaka 2010 Dayosisi Mkoani Arusha ilibadili jina na kuwa Dayosisi ya Kaskazini Kati, baada ya Serikali ya awamu ya tatu ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, kuamua kuugawa Mkoa wa Arusha na kutokeza mikoa ya Arusha na Manyara. Dayosisi iliendelea kuongozwa na Askofu Dkt. Thomas Olmorijoi Laiser hadi mwaka 2013 alipoitwa na Mungu mbinguni. Askofu wa pili wa Dayosisi ya Kaskazini Kati akawa Askofu Dkt. Solomon Jacob Massangwa ambaye ndiye Askofu hadi sasa.
Dayosisi ya Kaskazini Kati inatoa huduma ya injili ikimhudumia mwanadamu kiroho, kimwili na kiakili katika mikoa ya Arusha na Manyara isipokuwa maeneo ya Karatu, Mbulu na Meru.
Dayosisi ya Kaskazini Kati kwa sasa ina Majimbo matano ambayo ni:- Arusha Mashariki, Arusha Magharibi, Maasai Kusini, Maasai Kaskazini na Babati. Dayosisi hii ina Sharika 80, Mitaa 920, na Washarika wanaokaribia 300,000. Dayosisi ina Hospitali 3 Zahanati 8, Hoteli 1 ya kitalii, kituo cha mikutano cha Oldoinyosambu, shule za msingi 3, Shule za Sekondari 8 na Vyuo vya Ufundi 2.
Dayosisi ya Kaskazini Kati ina upana mkubwa unaochukua mikoa miwili yaani Arusha na Manyara. Kwa Upande wa Kaskazini, imepakana na nchi ya Kenya. Kwa upande wa Magharibi, imepakana na Dayosisi ya Mkoani Mara, Mashariki ya Ziwa Victoria, Mbulu na Jimbo la Karatu la Dayosisi ya Kaskazini. Kwa upande wa Kusini, imepakana na Dayosisi ya Dodoma na Morogoro. Kwa upande wa Mashariki, imepakana na Dayosisi ya Meru, Kaskazini, Mwanga, Pare na Kaskazini Mashariki.
MAONO YA DAYOSISI NA UTUME WAKE
Maono ya dayosisi ni kama yafuatavyo:
“Watu wenye furaha,amani na tumaini la kuurithi uzima wa milele kupitia Yesu Kristo“
UTUME WA DAYOSISI(MISSION)ni
“Kumuudumia mtu kikamilifu kiroho,kiakili na kimwili”
Muundo Wa Dayosisi Kiutendaji
